Friday, October 7, 2011

IFAHAMU HUDUMA YA SIFA NA KUABUDU

JAMBO LA MSINGI KUZINGATIA KWA WAIMBAJI/VIONGOZI WA SIFA

September 24, 2011


‘Ni ujumbe muhimu kwa kila Muimbaji kusoma’

Zaburi 150:1 “Haleluya, Msifuni Mungu katika patakatifu pake; msifuni katika anga la uweza wake”. Sehemu kubwa ya makanisa hapa duniani yana utaratibu au vipindi vya kumsifu na kumuabudu Mungu. Na katika makanisa hayo kuna viongozi au wambishaji wa nyimbo hizo za kusifu na kuabudu, na kwa taratibu za makanisa mengi mara nyingi sifa na kuabudu hutangulia mahubiri au mafundisho.

Naam sifa ni moja ya ibada ambazo kama watu watamaanisha ‘kumsifu Mungu’ toka ndani yao, tena wakiwa katika hali ya utakatifu, uwepo wa Bwana utashuka katikati yao na kuwahudumia. Siku moja nikiwa nimelala nilisikia sauti ikiniuliza maswali yafuatayo;

  • Je mnafahamu nini maana ya uiambaji?
  • Je mnajua sifa na kuabdudu zinaleta matokeo gani zinapoimbwa katika utakatifu?

Baada ya maswali haya ndipo ikaja picha ya dada mmoja Muimbaji aliyekuwa anaimba huku anamtukana Mungu. Watu wanazama wakidhani Mungu anawatembelea kumbe adui yumo katikati ya sifa kupitia mtu wake.

Baada ya kusikia maswali haya na kuona picha ya yule dada (maana namfahamu) moyo wangu uliumia sana. Naam ni dada ambaye ni mmoja wa waimbaji wazuri sana na amekuwa akimtumikia Bwana kwa nguvu zake nyingi iwe ni miukutano ya nje au ndani ya kanisa.

Katika kanisa lao dada huyu alikuwa ni mtu anayeaminiwa sana na Mchungaji wake na kanisa pia kwa ujumla kutokana na uimbaji wake. Moyoni mwangu niliwaza sana je ni kwa jinsi gani dada yule alikuwa anamtukana Bwana katika uimbaji wake? Je hii ina maana wakati watu wamezama kwenye sifa yeye husema maneno ya kumtukana Bwana? Nikagundua la hasha lazima kuna maana nyingine ya ndani na pana zaidi ambayo sikuwa naifahamu.

Nilipoanza kufuatilia ni kwa namna gani anamtukana Mungu kupitia uimbaji wake, ndipo Bwana alinijulisha siri iliyofichika. Bwana aliniletea maisha ya sirini ya yule dada ambayo hakuna kiongozi wa lile kanisa hata jimbo alikuwa anayajua. Wao walikuwa wakibarikiwa tu na uimbaji wake, wasijue kwamba ana siri zake nyingi mbaya ambazo huzitenda. Naam yule dada alikuwa ni Muasherati (Mzinzi). Upande mmoja alikuwa anamtumikia Mungu na upande wa pili akawa anamtumikia Shetani, kwa hiyo alikuwa vuguvugu kama Ufunuo wa Yohana 3:16 isemavyo.

Baada ya kujua jambo hilo ndipo Bwana alipozidi kunisemesha kupitia maandiko akisema, ‘hivi ndivyo ninavyotukanwa kila siku na watu hawa. Maisha yao yananuka dhambi, na viongozi wanawaamini watu hawa kiasi cha kuwaruhusu waongoze ibada za sifa. Mimi Mungu nakaa katika utakatifu na si dhambi’.

Baadhi ya waimbaji haya ndiyo wanayofanya katika makanisa yetu, wakichanganya mambo. Kitendo cha wao kuaminiwa, kupendwa na Wachungaji na watu pia kimewafanya kuwa na kiburi. Naam wapo waimbaji ambao ni walevi, wazinzi, waongo nk ambao siku za ibada ndio wanaotuongoza katika sifa. Sikia kanisa watu wa namna hii wanamtukana Mungu, ni machukizo makubwa.

Ni hatari kubwa sana kwa mtu kujiamini ukaendesha ibada wakati upande wa pili unatenda maovu, naam tambua kwamba kwa kufanya hivyo unamtukana Mungu. Nakusihi kwa huruma zake Kristo Yesu amua kuacha machafu hayo na kisha rudi katika hali ya utakatifu uwaongoze watu katika kumsifu Mungu. Naam zingatia jambo hili, ili uweze kuleta ladha ya sifa ambayo Bwana amekusudia watu waipate kupitia wewe.

Kumbuka kiburi hutangulia anguko, hii ina maana penye kiburi pana anguko. Namna watu wanavyokusifu kwa sababu ya uimbaji wako bila kujua matendo yako ya gizani ni kukupalia makaa ya hukumu yako. Laiti wangejua maisha yako ya upande wa pili yakoje wangekukwepa pengine kukufukuza. Sasa hao ni wanadamu ambao wengi hawajui, lakini Mungu anajua, tafadhali badilisha tabia yako kabla Mungu hajakutapika.

Yule dada alijiamini sana kutokana na huduma yake hiyo hali akijua hakuna mtu anayejua siri zake. Naam siku nilipomtafuta na kisha kumweleza mambo yake ya siri alilia sana kwa uchungu mwingi, ndipo akaniambia Mtumishi nilikuwa naficha jambo hili kutokana na umaarufu wangu, kwani niliogopa watu wakijua itakuwa ni aibu kubwa kwangu.

Hebu tufikiri kwa pamoja, huyu dada aliogopa kuaibika, lakini hakuona kwamba ni tatizo kumuabisha Mungu, naam si kumuabisha tu Mungu bali zaidi kumtukana. Maana leo mwimbaji huyu analala na mwanaume asiye mumewe, halafu Jumapili ndiyo anaongoza sifa, je si matusi haya kwa Mungu wetu. Naam laiti ungejua jinsi Mungu alivyo Mtakatifu usingegusa hata vyombo vya ibada, maana unavitia unajisi.

Kutokana na watu wengi kutokujua matokeo ambayo Mungu amekusudia kupitia uimbaji, wengi huishia kubarikiwa na kiwango kile cha sifa, wasijue kwamba laiti viongozi/waimbaji hawa wa sifa wangekaaa vizuri na Mungu wao, basi sifa pekee zingetosha kuleta uponyaji, kufunguliwa, ujazo wa Roho Mtakatifu nk.

Naam usipobadilika, ukaendelea na tabia hii, basi tegemea kile kilichotokea kwa watoto wa Haruni wakiwa madhabahuni kitatokea na kwako (Mambo ya Walawi 10:1-3). Maana kwa kitendo cha wao kuendesha ibada bila utakatifu, Mungu aliwapiga wote wawili wakafa papo hapo. Na baada ya kifo chao ndipo Musa akasema Jambo hili ni hilo BWANA alilonena akisema, Nitatakaswa mimi katika hao wanikaribiao. Tafsiri ya GNB inasema Then Moses said to Aaron, “This is what the LORD was speaking about when he said, ‘All who serve me must respect my holiness; I will reveal my glory to my people.

Naam huu ni wito kwa kanisa kwamba ni vizuri tujifunze kuwaombea sana waimbaji wetu, tukijua kwamba Shetani anatafuta sana kupitia kwa hao ili kuvuruga kile ambacho Mungu angefanya kama wangekaa katika hali ya utakatifu. Uimbaji ni ibada ya msingi na muhimu kama ilivyo neno pia. Hivyo waimbaji wanapaswa kufanya maandalizi kila iitwapo leo na kuzingatia utakatifu, ili kuongoza watu kumsifu Mungu katika roho na kweli.

Ni imani yangu kwamba maonyo haya katika Bwana yatakusaidia kurekebisha njia zako ili upate kuwa mtumishi mzuri wa Bwana katika nafasi ambayo Bwana amekuitia.

Neema ya Bwana iwe nawe siku zote.

No comments:

Post a Comment