Wednesday, April 11, 2012

Kanumba alitabiri ‘kifo’ chake

Msanii maarufu wa filamu, Steven Kanumba

Joachim Mushi

MSANII maarufu wa filamu, Steven Kanumba aliyezikwa leo jijini Dar es Salaam katika makaburi ya Kinondoni inasadikika kuwa alitabiri kifo chake siku kadhaa kabla ya kifo hicho.

Kanumba ambaye taarifa za awali za madaktari zinasema kifo chake kimetokana na mtikisiko wa ubongo alioupata baada ya kutokea mzozo na mpenzi wake nyumbani kwake Sinza Vatican hivi karibuni, rafiki zake wa karibu wanasema ametabiri kifo hicho katika filamu yake mpya ya ‘Love is Power’ ambayo bado haijaingia sokoni.

Akielezea leo mmoja wa rafiki zake ambaye ameshiriki katika utengenezaji wa filamu hiyo amesema katika filamu yake mpya ameigiza kifo ambacho alikipata baada ya kutokea mvutano kati yake na mkewe kwenye mchezo huo.

“Ukiangalia kwa makini katika picha hiyo unaweza kusema Kanumba kajitabiria kifo, maana matendo yote ambayo ameyaingiza katika filamu yake mpya ndiyo yaliyomtokea katika kifo chake halisi,” alisema mtu huyo.

Alisema katika filamu hiyo Kanumba ameigiza kujitolea figo kwa mke wake ambaye baadaye alikuja kumsaliti kwa kutoka nje ya ndoa na baada ya msanii huyo nyota kubaini uliibuka mzozo ambao ulisababisha kuwepo na ugomvi na mkewe lakini aliposukumwa na mkewe alianguka na kufa, jambo ambalo leo limetokea kweli katika mazingira ya kifo chake halisi.

Taarifa zaidi zinasema daktari ambaye alikuja kumtibu nyumbani kwake baada ya kuanguka juzi kabla ya mauti kumkuta ndiye aliyeigiza katika filamu hiyo mpya ya ‘Love is Power’, huku msanii ambaye pia amecheza kipande cha filamu kushuhudia kifo cha Kanumba ndiye juzi aliifunua maiti yake kwenye jokofu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH).

Mwili wa Kanumba umezikwa leo jijini Dar es Salaam mazishi ambayo yamekuwa ya kihistoria baada ya kuhudhuriwa na maelfu ya wakazi wa jiji, huku wengi wakianguka na kuzimia baada ya kushindwa kujizuia.

Kwa mujibu wa taarifa ya watoa huduma ya kwanza Chama cha Msalaba Mwekundu, tangua kuanza kwa shughuli za kuuaga mwili wa marehemu Kanumba viwanja vya Leaders Club hadi ukifikishwa katika makaburu ya Kinondoni takribani watu 200 walikuwa wamekwisha zimia na kupatiwa huduma ya kwanza na chama hicho.

Barabara ya kupitia makaburini ililazimika kufugwa kwa muda kutokana na wingi wa waombolezaji, huku Jeshi la Polisi likionekana kuzidiwa kuwadhibiti waombolezaji hali iliyosababishwa zoezi la kuuaga mwili wake kusitishwa na kupelekwa moja kwa moja makaburini, baada ya kumalizika kutoa salamu za mwisho viongozi mbalimbali wa juu Serikalini.

Makamu wa Rais wa Tanzania, Dk. Mohamed Gharib Bilal ndiye aliyewaongoza viongozi mbalimbali, wakiwemo baadhi ya mawaziri, wabunge, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam na viongozi wengine wa vyama na Serikali.

Hata hivyo wananchi wengi wameilalamikia Kamati ya Mazishi ya Kanumba kwa kile kushindwa kufanikisha Watanzania waliojitokeza kutoa salamu zao za mwisho kwa Kanumba licha ya wao kufika mapema katika viwanja vya Leaders Club.

Kanumba ambaye alizaliwa mwaka Januari 8, 1984 alifariki usiku wa kuamkia Aprili 7, 2012 baada ya kutokea mgogoro kati yake na mpenzi wake nyumbani kwake Sinza Vatican na kuzikwa Aprili 10, 2012 katika makaburi ya Kinondoni Dar es Salaam.
“Bwana ametoa na Bwana ametwaa jina lake lihimidiwe”

No comments:

Post a Comment